Siri ya Snura Kung’ang’ania kutoa video mpya Chura, baada ya video ya kwanza kufungiwa hii hapa


Kwa kawaida wasanii wengi ambao nyimbo zao hufungiwa, huachana nazo na kuendelea na nyingine, lakini kwa Snura imekuwa tofauti baada ya kuamua kukomaa hadi alipotimiza masharti yote na kuruhusiwa kuendelea na Chura wake.

“Nimekubaliana na maelekezo ya serikali na nimebadili video ya wimbo wangu wa Chura na sasa umeruhusiwa rasmi. Lakini najua watu wengi watakuwa wanajiuliza kwa nini nimeng’ang’ania huo wimbo? Kwanini nisingeendelea na nyingine nikaupotezea? Ukweli ni kwamba, Chura ndiyo kama utambulisho wangu.

“Bila Chura hakuna Snura, ndiyo maana nikaamua kutumia nguvu zangu zote kuurudisha. Kila mtu anafahamu kuwa Chura ndiyo wimbo wa kwanza wa Singeli kutamba kabla hata wanamuziki wengine hawajasikika.

“Wimbo huu uliniongezea mashabiki wa kila rika na Chura alikuwa gumzo kila kona hivyo kama mfanyabiashara sina budi kuweka mambo sawa ili nihakikishe naondoa hasara niliyopata wakati wimbo huo ulipofungiwa.

“Mashabiki bado wanaukubali sana na wanauhitaji, ndiyo maana nimeamua kutimiza yote urudi hewani. Angalia… wimbo ambao hausikiki kwenye redio wala runinga lakini upo midomoni mwa watu na huko mitaani bado unakiki kubwa.

“Halafu ukumbuke siyo hapa nchini pekee, hata nje ya mipaka ya nchi yetu. Juzi nimetoka Falme za Kiarabu, nilipotambulishwa nikatajwa kwa jina la Snura Chura kwa hiyo naanza kuvuka mipaka ya nchi na Chura wangu.”

eatv.tv