MAANDISHI YA TUNDU LISSU YANAHATARISHA AMANI NA UTULIVU WA NCHI ,SERIKALI YACHUKUA MAAMUZI MAZITO ZIDI YAKE

Akizungumza jana na vyombo vya Habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida ACP Thobias Sedoyeka, anasema bado wanaendelea kushirikiana na mamlaka mbalimbali ikiwemo TCRA ili kuweza kuthibitisha kuwa ule ujumbe uliokuwa unasambaa kwenye mitandao ya kijamii siku aliyokamatwa Mbunge huyo huko Ikungi-Jimbo la Singida Mashariki ni wa Mbunge Mh.Tundu Lissu.

RPC anasema wataangalia uwezekano wa kuwasiliana na TCRA ili kufungia "account" za Tundu Lissu mitandaoni, magroup ya mitandao ya kijamii aliyomo Tundu Lissu, kwani anachosha kwa kuitumia mitandao hiyo kueneza chuki dhidi ya jeshi la polisi, Serikali na Rais.

Hivyo, kama kuna uwezekano ni kumuondoa humo Tundu Lissu ili kuepusha uvunjifu wa amani unaosababishwa na maandishi yake ambayo yanahatarisha amani na utulivu wa nchi. RPC Sedoyeka anasema "Tunaangalia uwezekano wa kushirikiana na TCRA,wamfungie kabisa katika magroup ya mitandao ya kijamii,anakotumia kuandika lugha ya uchochezi na ya kuudhi dhidi ya serikali na uongozi uliopo"

ACP Sedoyeka anasema endapo watathibitisha aliandika Tundu Lissu,basi watamfungulia mashtaka ya uchochezi katika Mkoa wa Singida ambapo kosa hilo lilifanyika, kwani ujumbe ule umejaa uchochezi na uchonganishi,huku ukiwa na "maneno makali" ya kuipinga Serikali iliyopo madarakani.

Chanzo: Azam News(Azam Two)