Auawa kwa Kuiba Kuku..!!!

Mtu mmoja aliyejulikana kwa jina la Safari Bungate, miaka 51, mkazi wa Usagara, wilayani Misungwi mkoani Mwanza ameuawa na kundi la watu kwa kupigwa mawe na fimbo kwa madai ya kuiba kuku nyumbani kwa mtu. 


Taarifa ya jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza imesema kuwa tukio hilo limetokea tarehe 26.01.2017 majira ya saa 10 usiku katika kijiji cha Kanyelele, wakati mwenye nyumba bwana Tetema Mathias akiwa amelala  na familia yake.

Inadaiwa kuwa marehemu huyo alifika katika nyumba hiyo akaingia ndani kupitia dirishani na kuiba kuku mmoja, ndipo wakati alipokuwa anataka kuondoka mwenye nyumba huyo alimuona na kuanza kupiga yowe ya mwizi akiomba majirani wamsaidie kumkamata huku akimkibiza barabarani.

Inasemekana kuwa majirani waliamka na kufanikiwa kumkamata  marehemu akiwa na kuku amemshikilia kisha wakaanza kumpiga  kwa mawe na fimbo sehemu mbalimbali za mwili wake  kitendo kilichopelekea marehemu  kupoteza fahamu na baada ya muda mchache  alifariki dunia.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Ahmed Msangi amesema kuwa raia wema walitoa taarifa polisi ndipo askari walifika eneo la tukio na kukuta mtuhumiwa wa wizi akiwa tayari amefariki dunia.

Amesema mwili wa marehemu tayari umefanyiwa uchunguzi na daktari na kukabidhiwa kwa ndugu wa marehemu kwa ajili ya mazishi na kwamba mwenye nyumba Bwana Tetema Mathias anashikiliwa na jeshi la polisi kwa mahojiano zaidi