Jecha afunguka sababu za kufuta uchaguzi Zanzibar mwaka 2015

BAADA ya kimya kirefu, hatimaye Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salum Jecha amefunguka na kuelezea kuwa uamuzi aliouchukua wa kufuta uchaguzi wa Zanzibar wa mwaka 2015 baada ya kubainika kuwa na dosari, ulifanyika kwa kufuata taratibu, kanuni, Sheria na Katiba ya Zanzibar.

Jecha aliyasema hayo wakati akihojiwa na kipindi cha Funguka, kinachorushwa na Kituo cha Televisheni ya Azam na kusisitiza kuwa, hana wasiwasi wala hofu yoyote kwa hatua hiyo, aliyoichukua ya kufuta uchaguzi kwa kuwa ilifuata misingi yote ya Sheria na Katiba.

Pamoja na kwamba alikataa kujibu kwa undani kuhusu hatua yake hiyo na kusisitiza kuwa mengi atayabainisha kwenye taarifa ya tume, alisisitiza kuwa hakuwahi kutumika na chama chochote wala kuwasiliana na Rais Ali Mohammed Shein kama inavyodhaniwa na wengi. “Haya yote yataonekana kwenye taarifa ya uchaguzi, siwezi kuongea hapa sasa ila kiukweli utaratibu ulifuatwa. Matokeo yalifutwa kutokana na dosari zilizojitokeza ikiwemo baadhi ya matokeo kujulikana kabla na kusababisha baadhi ya vyama kulalamika,” alisisitiza Jecha.

Alieleza kuwa matatizo na dosari za uchaguzi huo, yalianza kujitokea katika kipindi cha kupokea matokeo ambapo matokeo yalitoka katika maeneo ya Unguja, hayakubainika kuwa na matatizo, isipokuwa kwa matokeo yalitoka katika maeneo ya Pemba.

Alisema katika kura hizo za Pemba, ilibainika kuwa utaratibu wa kiufundi ulifanyika kuharibu matokeo ya hesabu za kura baada ya kufanyika urekebishaji wa kasoro wa mambo, ambayo hayakutakiwa yafanywe nje ya sheria za uchaguzi.

Alisema baada ya kutokea kwa dosari hizo, kwa upande wa tume kupitia yeye, iliamua kufuta uchaguzi mzima ili kuepusha vurugu na mgongano wa kisiasa huku Polisi ikifanya uchunguzi kuwabaini wahusika waliosababisha dosari hizo katika matokeo ya uchaguzi. #PeruziNaKudadisi #HabariLeo