Jeshi la Polisi Dar laua majambazi, lakamata wauza shisha



Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewaua watu wawili wanaodaiwa kuwa ni majambazi na kukamata silaha pamoja na watuhumiwa kadhaa wa matukio ya kihalifu wakiwemo 7 wanaotuhumiwa kutengeneza kadi 7 za bandia za chanjo ya homa ya manjano

Akizungumza na vyombo vya habari, jana Jijini Dar es Salaam, Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, CP Simon Sirro alisema, mnamo tarehe 23 mwezi wa kwanza mwaka 2017 majambazi hao walitekeleza tukio la mauaji na kupora kiasi cha shilingi milioni 1 na laki 3 huko Boko Basihaya na polisi iliwasaka na kuwakamata na wakakiri kutenda mauaji hayo na kwamba walipojaribu kutoroka ndipo walipouawa.

Akielezea kukamatwa kwa watu 7 wanaodaiwa kutengeneza kadi bandia za homa ya manjano ambazo mtu hupaswa kuchomwa chanjo hiyo kabla ya kusafiri nje ya nchi, Kamisha Sirro alisema, watu hao wamekuwa wakitoa kadi hizo na kudai fedha nyingi kinyume cha sheria.
Jeshi hilo pia limewakamata watuhumiwa 92 wa makosa mbalimbali, ikiwemo wizi wa magari na pikipiki, watengenezaji wa gongo, shisha na uuzaji wa bangi.

Pia limekusanya zaidi ya Shilingi milioni 918, kwa ukamataji wa makosa ya usalama barabarani katika kipindi cha siku 10.